Quintel Blogger theme

A free Premium Blogger theme from newbloggerthemes.com

Saturday, August 18, 2012

MAJOGOO WA JIJI WATAWIKA MSIMU HUU....?


MAJOGOO WA JIJI WATAWIKA MSIMU HUU…...?
Kwa kawaida binadamu akisikia kiu hutafuta maji popote pale yalipo.Na mara maji yakikosekana ,binadamu  huyu hutamani kunywa chochote kile kilichopo mbele yake ilimradi kiwe ni kimiminika ili kukata kiu aliyonayo.
 Hakika kwa mfano huu wa kiu na maji kwa binadamu ndivyo navyouona kwa mashabiki wa klabu ya Liverpool ya nchini Uingereza.Kwani kwa muda mrefu sana mashabiki hawa wamevumilia kiu ya muda mrefu waliyokuwa nayo ya kutokuwa na vikombe kwa takribani miaka 22 sasa.
Ukibahatika kumuuliza shabiki yeyote yule wa klabu hii ni kitu gani anachotamani kukishuhudia katika klabu hiyo ya Liverpool basi hatosita kukwambia kuwa kiu yake itamalizwa kwa klabu hiyo kuchukua vikombe hasa ubingwa wa ligi kuu wa nchini Uingereza.
                                                                                                          
Tangu wachukue ubingwa wa iliyokuwa ligi daraja la kwanza (kwa sasa ligi kuu) nchini Uingereza mwaka 1990, Liverpool bado inahangaika mno kuupata ubingwa wa ligi kuu ya soka wa nchi hiyo.Kwani ni miaka takribani 22 sasa ambapo mashabiki wa Liverpool wamekuwa wakiusikia ubingwa huo wa ligi kuu kwa vilabu vingine kama Manchester United,Chelsea,Arsenal na sasa matajiri wa jiji la Manchester nawazungumzia Manchester City.
Hakika wapenzi wa kabumbu wataungana nami katika hili kuwa tangu Liverpool wautwae ubingwa wa iliyokuwa ligi daraja la kwanza(kwa sasa ligi kuu) mwaka 1990, mpaka sasa wanaliverpool na wapenda kabumbu duniani wameshuhudia vizazi vingi vikipita pasipo kufanikiwa kuchukua ubingwa wa ligi kuu nchini Uingereza ingawa Liverpool wamekuwa wakishinda makombe mengine mbali na ligi kuu kama kombe la chama cha mpira wa miguu nchini Uingereza(kombe la FA),kombe la ligi maarufu kama(Carling Cup) na klabu bingwa barani ulaya maarufu kama(UEFA Champions League).
Tumepata kushuhudia vizazi vya wachezaji kama Steven Mc Manaman,Jamie Redknap,Michael Owen,Robie Fowler,Steven Gerrad mpaka sasa kizazi cha akina Suarez,Joe Allen,Raheem Sterling ,Pacheco na Jonjo.Vizazi vyote hivyo nilivyotaja,wengi wa wachezaji waliondoka katika klabu hiyo pasipokuwa na ile medali ya ubingwa wa ligi kuu ya nchini Uingereza.Hii imezidi kuwafanya mashabiki wa klabu hiyo ya Anfield kuwa na hamu kubwa sana ya ubingwa huo wa ligi.


Machungu ya mashabiki hawa pia yanaongezeka katika hali ya kwamba klabu hiyo ya Liverpool ilichukuliwa kama mabingwa wa kihistoria wa ligi kuu nchini Uingereza kabla ya mashetani wekundu nawazungumzia Manchester United kuipiku rekodi hiyo ya vijana hao wa Anfield na hivyo kuzidi kuongeza presha kwa mashabiki wa Merseyside.Liverpool wameuchukua ubingwa wa ligi ya Uingereza mara 18 wakati Manchester United wameutwaa ubingwa wa ligi kuu wa nchi hiyo mara 19.
Swali la kujiuliza ni kuwa,Je ni saa ya ukombozi kwa majogoo hao wa Liverpool chini ya kocha mpya Brendan Rodgers?
Haya ni mambo matano(5) ya kiufundi ambayo binafsi tunaweza kuyaona ama kuyashuhudia kwa klabu ya Liverpool chini ya kocha mpya Brendan Rodgers.
·         Kwanza timu pinzani zitegemee presha kubwa sana toka katika safu ya ushambuliaji ya Liverpool.Hiki ndicho nilichokiona msimu uliopita kwa klabu ya Swansea iliyokuwa na kocha Brendan Rodgers.Washambuliaji wa Swansea Luke Moore,Leroy Lita na Loveridge walikuwa wakiwasumbua sana mabeki wa timu pinzani kutokana presha walioipeleka kwa mabeki wa timu hizo pinzani.Presha hii ilionekana kwa washambuliaji hao kuonekana wakianzia kukaba kwa mbele ili kuwanyima mabeki nafasi ya kutoa pasi za viungo.Vivyo hivyo nategemea mno kuiona safu ya ushambuliaji ya akina Luis Suarez,Fabio Borin,Andrew Carol na Pacheco kufanya hivyo kwa mabeki kama Nemanja Vidic,John Terry,Vicent Kompany,Thomas Vermeleen na wengine wengi toka vilabu shiriki vya ligi kuu msimu huu ambayo ndiyo falsafa ya kocha Brendan Rodgers.
·         Tutegemee soka la pasi na timu kusogea mbele ya lango la wapinzani muda wote.Msimu uliopita wa (2011-12),klabu ya Swansea ilikuwa ni miongoni mwa vilabu vilivyoongoza kwa kupiga pasi kwa usahihi ndani ya mchezo katika ardhi ya Uingereza na nje ya mipaka ya Uingereza sanjari na timu kama Barcelona,Real Madria,Bayern Munich,Manchester United nk.Jumla ya pasi 2,111 zilipigwa na klabu hiyo huku pasi 2,107 zikipigwa na viungo wawili bora kabisa kwa sasa nchini Uingereza ambao ni Leon Briton na Joe Allen.
Takwimu zinaonesha kuwa Leon Briton alipiga pasi sahihi kwa 93% huku kiungo mwenzake Joe Allen akipiga pasi sahihi 91% katika mechi walizocheza msimu uliopita.Hakuna hata mchezaji mmoja wa klabu ya Liverpool aliyeweza kufikisha idadi hiyo ya pasi.Hii ina maana ya kwamba siyo nahodha Steven Gerrad,Lucas,Charlie Adam wala Jordan Hernderson walioweza kufikisha idadi kupiga pasi kwa usahihi ya viungo hao.Ila kujiunga kwa mchezaji Joe Allen kunako klabu hiyo ya Anfield kutaibadiri sura ya sehemu ya kiungo cha Liverpool katika msimu huu wa ligi ya Uingereza.

·         Tutegemee pia kasi nzuri katika sehemu za pembeni mwa uwanja(wings).Wakati akiwa na klabu ya Reading,kocha Brendan Rodgers aliweza kuwatumia mawinga Jimmy Kebbe na Joby McAnuff ambao waliweza kumsaidia katika falsafa yake ya kuhakikisha kuwa mawinga wanatumika katika mashambulizi ya klabu hiyo ya Reading.Akiwa na Swansea aliweza kuwapika vizuri mawinga Scott Sinclair,Nathan Dyer na Wayne Routledge katika kushambulia mabeki wa timu pinzani.
Liverpool hawakuwa na mawinga wenye kasi wa kariba ya Sinclair,Dyer na Routledge na hivyo kwa kiasi kikubwa kulidhoofisha sehemu ya ushambuliaji ya klabu hiyo ya Anfield kwani ni Luis Suarez pekee aliyekuwa katika fomu ya hali ya juu sana hasa wakati ambapo alikuwa akitokea pembeni kuingia ndani ya eneo la timu pinzani.Hivyo ujio wa Brendan Rodgers utaifufua sehenu hiyo ya pembeni ya Liverpool ikizingatiwa kuwa kuna uwepo wa mawinga asilia kama Stewart Downing,Rahim Sterling, na Joe Cole.

·         Liverpool hawatotegemea sana mashambulizi ya kushtukiza msimu huu kwa maana ya(counter attack) huku msisitizo ukiwa kushambulia kuanzia sehemu ya ulinzi.
Ukiwaangalia vizuri Swansea msimu uliopita,utagundua kuwa timu yao ilijengeka vizuri sana kimashambulizi kuanzia sehemu ya mabeki halafu viungo na mwisho ni washambuliaji.Mabeki kama nahodha Gary Monk,nahodha msaidizi Alan Tate,Chico na bila kumsahau Ashley Williams walikuwa wazuri katika kuanzisha mashambulizi ambayo yalipokelewa vizuri na viungo kama Joe Allen(amehamia Liverpool),Leon Briton,Scott Sinclair mpaka kwa washambuliaji Leroy Lita na Luke Moore.
Mfumo huo huo wa mashambulizi tunatarajia kuuona katika klabu ya Liverpool ambapo mabeki Daniel Agger,Sebastian Coates,Martin Sktel,Glen Johnson na wengineo wakianzisha mashambulizi na si kuwategemea kina Gerrard,Joe Allen,Charlie Adam na Luis Suarez pekee katika kuanzisha mashamulizi.
·         Tutegemee kuimarika kwa safu ya ushambuliaji kutokana na  kusajiliwa wachezaji wapya ili kusaidiana na Luis Suarez.
Sehemu ya ushambuliaji iliwaangusha sana Liverpool msimu uliopita.Katika sehemu hiyo ya ushambuliaji ni mchezaji mmoja tu aliyekuwa katika fomu ya hali ya juu sana pamoja na kukumbwa na rungu la chama cha soka nchini Uingereza(FA) la kufungiwa mechi nane(8) kutokana na kashfa ya ubaguzi kwa mchezaji wa Manchester United Patrice Evra namzungumzia Luis Suarez.Hakika Suarez alikuwa na mchango mkubwa sana kwa klabu hiyo ya Anfield msimu uliopita.Aliweza kuwazidi washambuliaji wengine kama Andrew Carol,Craig Bellamy na Dirk Kuyt.
- Suarez ndiye alikuwa mfungaji bora wa Liverpool msimu uliopita akifunga magoli kumi na moja (11).
- Suarez alishika nafasi ya pili kwa kupiga pasi za magoli kwa Liverpool nyuma ya kiungo Charlie Adam.Charlie alitoa pasi sita (6) za magoli wakati Suarez alitoa pasi (3) za magoli.
- Suarez aliongoza kwa kupiga mashuti langoni mwa timu pinzani huku akipiga mashuti 128 kati ya hayo mashuti 48 yakilenga goli.Bila kusahau kuwa Suarez ndiye mchezaji aliyefanyiwa madhambi(faulo) kuliko mchezaji yeyote pale Liverpool akifanyiwa faulo mara 74.
Kwa ujumla sehemu ya ushambuliaji katika klabu ya Liverpool ilimhitaji mchezaji atakayesaidiana na Luis Suarez hasa katika eneo la theluthi ya mwisho ya eneo la wapinzani maarufu kama(final third).Hivyo ujio wa Fabio Borini,uwepo wa Andrew Carol na makinda kama Pacheco na Raheem Sterling utampunguzia Suarez kwa kiasi kikubwa mzigo aliokuwa nao msimu uliopita pale Anfield.Hata hivyo usajiri bado unaendelea na hivyo tunaweza kushuhudia majina mengine yakitua pale Anfield.

Hivyo ndivyo navyoitazama Liverpool chini ya kocha Brendan Rodgers kwa msimu mpya wa 2012-13.

KILA LA KHERI LIVERPOOL KATIKA MSIMU HUU MPYA WA LIGI KUU YA SOKA NCHINI UINGEREZA

0 comments:

Post a Comment